Uongozi wa Wanawake na Samia

Scroll Down To Discover
Font size:

Urithi wa Samia Katika Kuwawezesha Wanawake wa Tanzania

Kila kona ya Tanzania ilipiga vifijo na vigeregere baada ya nchi kuwa na Rais wa kwanza Mwanamke. Wengi walihusianisha tukio hili na mapinduzi ya kijinsia. Wasichana wadogo nao walipata mfano bora wa kufikia ndoto zao. Tangu alipoingia madarakani, Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa kiongozi anayevunja mipaka katika kusukuma mbele usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake nchini Tanzania. Rais Samia hajavunja tuu rekodi ya kihistoria ya kuwa Rais wa kwanza mwanamke baada ya awamu tano tangu nchi ipate uhuru, bali pia ameweka historia ya mabadiliko makubwa, kwani anaendelea kuongoza sera na mipango inayowainua wanawake katika sekta zote za jamii. Jitihada za Rais Samia zimeunda mazingira wezeshi kwa wanawake kuibuka kama viongozi katika siasa, biashara, na jamii, kumfanya kuwa mtetezi halisi wa usawa wa kijinsia Tanzania.

Uwezeshaji wa Wanawake Kisiasa

Licha ya Mhe. Rais Dkt. Samia kuamini katika jitihada binafsi na uzoefu wa kazi, ametoa kipaumbele kwa ushiriki wa wanawake katika uongozi na maamuzi, hasa kwenye siasa. Chini ya uongozi wake, wanawake wengi zaidi wamepewa nafasi za juu serikalini, ikiwemo wizara na mikoa. Baraza lake la mawaziri lina uwakilishi mkubwa wa wanawake, huku wizara muhimu kama Fedha, Elimu, na Afya zikiongozwa na wanawake. Kwa kuwateua wanawake katika nafasi hizi muhimu, Samia ameonyesha dhamira yake ya kukuza uongozi wa wanawake na kuhakikisha sauti zao zinasikika katika ngazi za juu za utawala. Hii inaendelea kuwa moja ya mafanikio makubwa sana katika nchi iliyoaminika kuwa na mfumo dume. Uwepo wa wanawake kwenye sekta hizi muhimu unaonyesha jinsi changamoto zinazowakumba wanawake zimepata wawakilishi sahihi wanaoweza kujiweka kwenye viatu vyao.

Mfano Hai: Jenista Mhagama

Jenista Mhagama, Waziri wa Afya wa Tanzania, ni mmoja wa wanawake waliostawi chini ya uongozi wa Rais Samia. Ufanisi wake katika sekta ya afya unathibitishwa na juhudi zake za kuimarisha mfumo wa afya nchini. Uwezo wake wa kuleta ushirikiano kati ya serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali, na jamii umeweza kuboresha hali ya afya nchini Tanzania na kuhakikisha kwamba masuala ya wanawake yanapewa kipaumbele katika sera za afya. Unaweza kujiuliza kwanini wanawake katika sekta ya afya wanapaswa kuwa viongozi, hali ni kwamba wao ndio msingi wa jamii na wanaotazama na kuhudumia familia, hususan kwenye masuala ya afya. Wahudhuriaji wakubwa katika vituo vya afya ni wanawake. Wanapokuwa katika nafasi za uongozi wa sekta ya afya, wanawake wana nafasi nzuri ya kuimarisha sera zinazohusiana na afya ya uzazi, ikiwa ni pamoja na huduma bora kwa wajawazito, uzazi wa mpango, na huduma kwa watoto wachanga.

Kuwasaidia Wanawake Katika Biashara na Ujasiriamali

Serikali ya Rais Samia imetekeleza sera zinazolenga kuimarisha uwezo wa kiuchumi wa wanawake kwa kuwaunga mkono wajasiriamali wanawake na wamiliki wa biashara ndogo ndogo. Ameongoza mipango inayotoa rasilimali za kifedha na programu za kujenga uwezo kwa wanawake wafanyabiashara, hasa katika maeneo ya vijijini ambako upatikanaji wa mtaji umekuwa changamoto. Chini ya uongozi wake, Tanzania pia imeona kuongezeka kwa vyama vya ushirika vinavyoongozwa na wanawake na programu za mikopo midogo midogo, ambazo zinatoa zana muhimu kwa wanawake kufanikiwa katika ujasiriamali. Programu kama hizi zimewasaidia wanawake kupata masoko, kupokea mafunzo ya usimamizi wa biashara, na kukuza biashara zao, na hivyo kuchangia kwa kiasi kikubwa kwenye uchumi wa taifa.

Mfano Hai: Angel

Angel, mfanya biashara mdogo anayetengeneza mvinyo kwa kutumia nyanya kutoka Iringa, alinufaika na mojawapo ya programu za BBT zinazoungwa mkono na serikali. Kwa msaada wa kifedha na mafunzo aliyopata, Angel alihama kutoka utengenezaji mdogo wa mvinyo na kuingia katika uzalishaji mkubwa. Safari yake inaonyesha uwezeshaji ambao Rais Samia amefanikisha, na kuthibitisha kwamba wanawake wanaweza kufanikiwa katika ujasiriamali wanapopata fursa sahihi.

Utetezi wa Haki za Wanawake na Usawa wa Kijinsia

Rais Samia amekuwa mtetezi mkubwa wa haki za wanawake, akihakikisha kwamba usawa wa kijinsia unakuwa kipaumbele cha sera za taifa. Serikali yake inaendelea kufanya kazi ya kurekebisha sheria na sera zinazowabagua wanawake na wasichana, ikiwa ni pamoja na zile zinazohusiana na elimu, umiliki wa ardhi, na ukatili wa kijinsia.

Kuvunja Vikwazo Katika Elimu kwa Wasichana

Hivi sasa, kila mkoa wa Tanzania unajengwa shule ya sekondari ya bweni kwa wasichana. Jitihada hizi zinaendelea chini ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuhakikisha wasichana wanapata elimu bora bila vikwazo. Rais Samia ameweka mkazo katika kuboresha upatikanaji wa elimu kwa wasichana, kipengele muhimu cha kuwawezesha kizazi kijacho cha viongozi wanawake. Ameweka kipaumbele sera zinazolenga kuwaweka wasichana shuleni, hasa katika jamii zilizoko pembezoni, kwa kuhakikisha kuwa wasichana wajawazito na wamama vijana wanapewa nafasi ya kuendelea na masomo yao. Mtazamo huu wa maendeleo umefanya elimu kuwa jumuishi zaidi na kufungua milango kwa wasichana wengi kufikia uwezo wao.

Kumtua Mama Ndoo Kichwani

Serikali ya Rais Samia imewekeza katika miradi mikubwa ya maji vijijini na mijini. Lengo kuu ni kuhakikisha maji safi na salama yanapatikana karibu na makazi ya watu, hivyo kuwapunguzia wanawake safari ndefu na za kila siku za kutafuta maji. Kwa mfano, serikali ilitenga zaidi ya TSh bilioni 700 katika mwaka wa fedha wa 2022/2023 kwa ajili ya miradi ya maji vijijini na mijini. Hii ni ongezeko kubwa ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

Hitimisho

Jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kukuza usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake zinabadilisha mustakabali wa Tanzania. Kupitia sera na mipango yake, ametengeneza fursa kwa wanawake kufanikiwa katika siasa, biashara, elimu, na zaidi. Kadiri urithi wake unavyoendelea, ni wazi kwamba Samia anaacha alama isiyofutika katika maendeleo ya Tanzania kuelekea usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake. Kuanzia kuwa mfano wa kuigwa kwa mabinti wadogo, wasichana, na wanawake katika gurudumu la uongozi, uwezo wake wa kusimama kidete na kuachilia mbali changamoto mbalimbali zinazowakabili wanawake katika uongozi umeendelea kuwapa ari wanawake wengi zaidi kufikiria kuwania nafasi hizi.

or

For faster login or register use your social account.

Connect with Facebook