Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan ameagiza kuwa Tamasha la Kizimkazi la kila mwaka liingizwe rasmi kwenye orodha ya matukio yanayochangia kukuza utalii nchini Tanzania. Hatua hii inalenga kuimarisha hadhi ya tamasha hilo kitaifa na kimataifa. Akihutubia kwenye kilele cha Tamasha la Kizimkazi la mwaka 2024, Rais Hassan alisisitiza kwamba tamasha hilo limetimiza malengo yake ya kuendeleza umoja, maendeleo, na uhifadhi wa utamaduni.
Rais Hassan alibainisha kwamba tamasha hili sio tu ni fursa ya kufurahia utamaduni, bali pia ni kichocheo cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii. "Lengo letu ni kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii, lakini zaidi ya hapo ni kuwaunganisha watu, kudumisha udugu, mila, na desturi," alisema Rais Dkt Samia Suluhu Hassan.

Kwa hatua ya hii ya kujumlisha tamasha hili katika kalenda rasmi ya utalii ya Tanzania, Tamasha la Kizimkazi linatarajiwa kuwa tukio kubwa zaidi katika sekta ya utalii kwa miaka ijayo. Kulingana na takwimu za Benki Kuu ya Tanzania, kufikia mwishoni mwa Juni 2024, idadi ya watalii imeongezeka hadi 1,994,242 ikilinganishwa na 1,638,846 waliorekodiwa Juni 2023. Katika kipindi hicho, mapato yaliyopatikana kwenye shughuli za usafiri yalifikia dola bilioni 3.6 kutoka dola bilioni 2.9. Lengo la nchi ni kufikia dola bilioni 6 ifikapo mwaka 2025.
Rais Hassan alisisitiza kwamba tamasha hili lina umuhimu mkubwa, si tu kama sherehe, bali pia kama kichocheo cha maendeleo ya jamii. Miradi mbalimbali ya maendeleo Kizimkazi imepata msukumo mkubwa kipindi cha tamasha hili, huku wadau wakishiriki kikamilifu katika ukuaji wa eneo hilo. Rais Samia pia aliwataka wananchi kuendelea kushirikiana na kufuatilia utekelezaji wa miradi iliyokubaliwa. "Kwa kufuatilia na kusimamia yote tuliyokubaliana katika kipindi hiki, watu lazima wawe mstari wa mbele, wakionyesha kuwa Kizimkazi imeitikia na hakuna aliyebaki nyuma," alisema.
Akizungumza kwa niaba ya kamati ya maandalizi, Bw. Ahmed Hamisi alielezea mafanikio ya tamasha hilo, hasa katika suala la miradi ya maendeleo iliyofadhiliwa na wadau mbalimbali kama vile hospitali, masoko, shule, na kituo cha michezo katika eneo hilo. Alitoa shukrani kwa serikali ya Zanzibar, inayoongozwa na Rais Hussein Ali Mwinyi, kwa kuahidi kushughulikia changamoto muhimu zinazoikabili jamii hiyo.
Katika tukio la kufurahisha wakati wa Tamasha la Kizimkazi, Rais Hassan alifichua sababu ya kumpa jina la kiongozi wa upinzani, Tundu Lissu, moja ya simba katika maonesho ya wanyamapori ya tamasha hilo. Alisimulia jinsi alivyoshtushwa na asili ya simba mmoja aliyekuwa mkali na asiye na utulivu. "Niliwauliza waandaaji kama simba huyo alikuwa na jina, na waliposema hana, niliwaambia wampatie jina la mwanangu, Tundu Lissu, kwa sababu alikuwa mkali na asiye na utulivu kama Tundu Lissu," alisema Rais Dkt Samia Suluhu Hassan. Kauli hiyo iliibua vicheko na makofi kutoka kwa hadhira.
Kama inavyofahamika kuwa Tundu Lissu, ni kiongozi mashuhuri zaidi wa upinzani anayetambulika kwa msimamo wake thabiti na wa wazi dhidi ya serikali.
